Ijumaa, 2 Desemba 2016

WATANZANIA WATAKIWA KUSHIKAMANA NA KUIPENDA NCHI YAO


ft
Na. Jovina Bujulu – Maelezo
 
WATANZANIA wametakiwa kushikamana, kupendana na kulinda rasilimali zao kwani wao ndio wenye mamlaka ya kuendesha nchi yao.
 
Wito huo umetolewa leo jijini Dar es slaam na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Idara ya Sayansi na Siasa Dkt. Bashiru Ally  wakati wa mahojiano na Mwandishi wa habari kuhusu mafanikio ya miaka 55 ya uhuru wa Tanzania ambayo yatafikia kilele tarehe 9 Desemba.
 
Akizungumzia mafanikio ambayo nchi imefikia tangu ilipopata uhuru mwaka 1961 alisema kuwa Tanzania imefanikiwa kujenga umoja wa kitaifa hasa kwa kutumia lugha ya Kiswahili katika shughuli mbalimbali za Kitaifa na kimataifa.
 
“Matumizi ya Kiswahili katika kazi za kitaaluma, kibiashara na nyanja za sayansi yameimarisha umoja wa kitaifa” alisema Dkt. Bashiru.
 
Aidha Dkt. Bashiru alimpongeza Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutumia lugha ya Kiswahili katika shughuli mbalimbali za kitaifa na kimataifa kwa kuwa lugha hiyo ina utajiri wa maneno hivyo ikutumika vizuri Tanzania itapiga hatua zaidi na kuimarisha mshikamano wa kitaifa.
 
Akizungumzia suala la nchi kuelekea uchumi wa viwanda vidogo na viwanda vya kati Dkt. Bashiru alisema kuwa ni vizuri viwanda vinavyoanzishwa  sehemu kubwa ya malighafi vikatumia rasilimali za nchini na vizingatie maslahi ya watanzania kwa misingi ya usawa, haki na utu ili vizalishe ajira kwa vijana wa Tanzania.
 
“Rais awaamini Watanzania ndiyo wazalishaji namba moja hasa wazalishaji wadogo na nguvu zielekezwe katika uzalishaji ili fedha zinazopatikana zielekezwe katika huduma za kijamii kama vile elimu, afya na maji”, aliongeza Dkt. Bashiru.
 
Kwa upande wa suala la nidhamu ,Dkt. Bashiru alisema kuwa kumekuwepo na mabadiliko makubwa kwa watumishi wa Umma ambapo wafanyakazi wanahi kazini, kutumia lugha nzuri na kupunguza vitendo vya kudai rushwa.
 
Alimpongeza Rais Dkt. Magufuli kwa juhudi anazozifanya za kukusanya mapato na kusimamia nidhamu ya matumizi ya fedha hizo na alimtaka asilegeze kamba katika kusimamia eneo la uzalishaji.
 
Alisema kuwa jitihada hizo ndio zimesaidia Shule kifurika wanafunzi kutokana na elimu bure, ongezeko la madawati mashuleni na mafanikio katika sekta ya afya na kilimo.
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni