CHUO CHA ARDHI CHATOA ZAWADI KWA WANAFUNZI 104 WALIOFAULU.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, 
Prof. Idrissa Mshoro (katikati kulia) akiteta jambo na Kaimu Naibu 
Makamu Mkuu wa Chuo hicho (Taaluma), Prof. Gabriel Kassenga(katikati 
kushoto), pembeni kulia ni Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa chuo hicho 
(Mipango, Fedha na Utawala),Prof. Robert Kiunsi, pembeni kushoto ni 
Maafisa Waandamizi wa chuo hicho. Shughuli hizo zimefanyika leo Jijini 
Dar es Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
Mmoja kati ya washindi wa jumla 
wenye alama za juu, Anyighwile Lwijiso akipokea zawadi kutoka kwa mmoja 
wa wafadhili ambao ni Kampuni ya Hightech System mara baada ya 
kutangazwa kuwa mshindi. Shughuli hizo zimefanyika leo Jijini Dar es 
Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Ardhi, 
Prof. Idrissa Mshoro akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa chuo 
na wanafunzi waliofanya vizuri kitaaluma wakati wa shughuli za ugawaji 
wa vyeti na zawadi kwa wanafunzi waliofaulu masomo mbalimbali 
uliofanyika leo Jijini Dar es Salaam katika viwanja vya chuo hicho.
…………………..
           Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.
Chuo Kikuu cha Ardhi kimetoa 
zawadi na tuzo kwa wanafunzi 104 waliofanya vizuri kitaaluma ili kutoa 
hamasa kwa wanafunzi wengine kuweka juhudi katika masomo.
Zawadi hizo zimetolewa leo Jijini 
Dar es Salaam na Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Idrissa Mshoro ambaye 
ametangaza kuwa jumla ya wanafunzi wanne kati ya waliofanya vizuri 
wamepata alama sawa hivyo kuibuka washindi wa jumla kwa mwaka 2016. 
Akisoma hotuba wakati wa sherehe 
hizo, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho (Taaluma), Prof. Gabriel 
Kassenga amesema kuwa sherehe hizo zimekuwa zikiwezeshwa na wadau 
mbalimbali waliojitoa kwa hali na mali kutoa zawadi na tuzo kwa 
wanafunzi waliofaulu vizuri kwenye vipengele mbalimbali vya taaluma 
hivyo amewasihi wadau hao kuendelee kuunga mkono jitihada zinazofanywa 
na wanafunzi hao ili kuwashawishi wanafunzi wengine kufanya vizuri.
“Zawadi mbalimbali zinazotolewa na
 wafadhili zimekua zikiwasaidia wanafunzi hawa kuongeza tija kwenye 
maisha yao ya kielimu na kiuchumi kwani wengi wao wamekuwa wakizitumia 
fedha hizo kama mitaji ya kufanyia biashara pindi wamalizapo masomo 
yao,”alisema Prof. Kassenga.
Amefafanua kuwa mwaka huu umekuwa 
wa tofauti kwani idadi ya wanafunzi wanawake na wanaume waliopata tuzo 
hizo iko sawa tofauti na miaka mitatu iliyopita ambapo wanawake walikua 
wakiongoza kwa asilimia 3.7 kwa kupata tuzo nyingi wakati wanaume wakiwa
 ni asilimia 2.2. 
Prof. Kassenga ametaja baadhi ya 
zawadi zilizotolewa na wafadhili walioshiriki katika shughuli hiyo kuwa 
ni vyeti, Kompyuta mpakato (laptop),vifaa vinavyotumika katika kupimaji 
wa ardhi pamoja na fedha taslimu.
Aidha, Prof. Kassenga ametoa rai 
kwa kwa wanafunzi wote waliomaliza chuoni hapo kuwa juhudi walizokuwa 
wakizionyesha wakati wa masomo waende wakaziendeleze katika jamii 
zinazowazunguka pamoja na kwenye shughuli mbalimbali za ujenzi wa Taifa 
ili wakawe mfano bora kwa vizazi vijavyo.
Kwa upande wake Emily Elandogo 
ambaye ni mmoja kati ya wanafunzi waliopewa zawadi hizo amewashukuru 
walimu wa chuo hicho kwa elimu wanayoitoa ambayo itakua ni chanzo cha 
kuwaletea maendeleo sehemu yoyote watakapokuwa pia ametoa ushauri kwa 
wanafunzi wenzake kuitumia vizuri elimu waliyoipata ili iweze kuwasaidia
 katika maisha yao.  
Mahafali ya Kumi ya chuo hicho 
yanategemewa kufanyika Disemba 3 mwaka huu katika viwanja va chuo hicho 
ambapo wahitimu wa shahada mbalimbali watatunukiwa stahili pamoja na 
vyeti vyao. 
                         MWISHO
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni