Jumanne, 24 Februari 2015

WALIOANDAMANA KUDAI AJIRA JKT WAFIKISHWA MAHAKAMANI LEO

Na Tinah Reuben

VIJANA sita waliokuwa katika mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) wanaodaiwa kupanga kuandamana mpaka kwa Rais Jakaya Kikwete kudai ajira,wamefikishwa leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Jijini Dar es Salaam.

Wakisomewa mashtaka yao na mwendesha mashtaka wa serikali,Tumaini Kwema mbele ya Hakimu Mkazi ,Frank Mushi alidai  kuwa,washtakiwa hao wanadaiwa kufanya fujo,kufanya mkusanyiko usiokuwa wa halali ili kuilazimisha serikali kuwapatia kazi na kushawishi kutenda makosa ya jinai kwa kuandamana mnamo Februari 15 mwaka huu eneo la Msimbazi Centre jijini Dar es salaam.

Washitakiwa hao ni George Gagris,Linus Immanuel,Pharas Owera,Emmanuel Richard,Ridhwan Brayson na Jacob Joseph.

 Baada ya kusomewa mashtaka na mwendesha mashtaka,Tumaini Kwema,watuhumiwa hao wote kwa pamoja walikana mashtaka hayo.

Washtakiwa hao wamerudishwa tena rumande kutokana na kutokidhi masharti na vigezo vya dhamana,kesi hiyo itatajwa tena Machi 6 mwaka huu.
 Baadhi ya vijana waliokuwa katika mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) wanaodaiwa kupanga kuandamana mpaka kwa Rais Jakaya Kikwete kudai ajira,wakiwa chini ya ulinzi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu,jijini Dar es salaam leo.
 Watuhumiwa hao wakipandishwa kwenye gari ya polisi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni