Jumatano, 4 Mei 2016

MHE. UMMY MWALIMU AELEZEA MIKAKATI YA SERIKALI KATIKA KUHAKIKISHA USAWA WA KIJINSIA KATIKA ELIMU

wm1 
Mke wa Rais Mstaafu na Mwenyekiti wa WAMA, Mama Salma Kikwete akisoma hotuba yake kwa wageni waalikwa na wahitimu wakati wa Sherehe za Mahafali ya kwanza ya Kidato cha Sita ya Shule ya WAMA- Nakayama.
wm2 
Kaimu Balozi wa Japan hapa nchini Bw. Hiroyuki KUBOTA akisoma hotuba yake wakati wa Sherehe za Mahafali
wm3 
Wahitimu wa Kidato cha Sita wa Shule ya Sekondari ya WAMA -Nakayama  katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa WAMA mara baada ya kumkabidhi Cheti cha Shukrani  kwa mchango wake katika maendeleo ya elimu yao.
wm4 
Wahitimu wa Kidato cha Sita wa Shule ya Sekondari WAMA- Nakayama wakionyesha maonyesho ya masomo kwa Mgeni Rasmi, Mhe. Ummy Mwalimu, Mwenyekiti wa WAMA, Mama Salma Kikwete pamoja na wageni waalikwa.
wm6 
Dr. Ramadhani Dau, Mwenyekiti wa Bodi ya Shule ya Sekondari ya WAMA- Nakayama akitoa neno la ukaribisho kwa wageni waalikwa katika Sherehe za mahafali ya Kidato cha sita  shule ya sekondari WAMA Nakayama
…………………………………………………………………………………………………
Na Philomena Marijani, WAMA Foundation
Serikali imechukua hatua maalum za kisera na   kimipango kuhakikisha  kunakuwa  na usawa wa kijinsia katika elimu, mafunzo, sayansi na teknolojia. Maelezo hayo yametolewa na  Mhe.Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto  wakati wa sherehe za Mahafali ya kwanza ya Kidato cha Sita ya Shule ya Sekondari ya WAMA- Nakayama yaliyofanyika mwishoni wa wiki katika ofisi za WAMA zilizopo Kawe, Dar es Salaam.
Mhe.Ummy Mwalimu ambaye alikuwa mgeni rasmi katika sherehe hizo amesema moja ya hatua hizo ni pamoja na kuongeza idadi  ya wasichana wanaopata elimu ya msingi ili kuwepo na idadi sawa ya wavulana na wasichana.
Aliongeza   kuwa kwa  mwaka 2008 serikali ilifanyia marekebisho Sheria ya Elimu na mafunzo ili kukidhi matakwa ya usawa wa kijinsia. “Baadhi ya maswala ambayo yamerekebishwa ili kuboresha  mazingira  ya shule yaweze kuwa rafiki kwa wasichana ni pamoja na kuhamasisha jamii kutoa chakula shuleni, kujenga mabweni na vyoo kwa ajili ya wasichana na pia kuongeza idadi ya walimu.  Wizara yangu pia imeandaa Sera ya Maendeleo ya Mtoto ya mwaka 2008 na Sheria ya Mtoto No.21 ya mwaka 2009 ambayo inasisitiza jamii kuzingatia utoaji wa haki za msingi kwa watoto, moja ya haki hizo ni haki ya kuendelezwa.” Alisema Mhe. Ummy Mwalimu.
Mhe. Mwalimu aliwashauri wahitimu wa WAMA-Nakayama  wasiridhike na elimu ya kidato cha sita  bali wajiendeleze kwa kujiunga na vyuo mbalimbali hapa nchini  na hatimaye serikali ipate viongozi wengi wanawake. 
Akiongea katika sherehe za mahafali hayo  Mke wa Rais Mstaafu na Mwenyekiti wa WAMA Mama Salma Kikwete  alisema Shule ya Sekondari ya WAMA- Nakayama ilianzishwa  ili kutoa mchango  katika Juhudi za Taifa za kumkomboa mwanamke  kwa kuwapatia fursa za  elimu bora ya sekondari watoto wa kike wanaotoka katika mazingira magumu wakiwemo yatima.
Taasisi inatambua kwamba ili mtoto wa kike aweze kupata mafanikio katika masomo yake ni muhimu kumjengea mazingira wezeshi ya kusomea na kuishi. Ndiyo maana tuliamua kuwajengea shule yenye mahitaji yote ya kupata elimu bora na pia kuepuka vishawishi mbalimbali vinavyoweza kupelekea kukatisha masomo. Alisema Mama Kikwete.
Mama Kikwete aliwashukuru wadau wote  ambao wamekuwa wakitoa misaada mbalimbali tangu kuanzishwa kwa shule ya WAMA- Nakayama na kusema ushirikiano huo umesaidia kufanikisha ndoto ya kuwasaidia watoto wa kike  na matunda yake yanaonekana kwa wanafunzi wanaohitimu kidato cha sita.
Akisoma hotuba yake Kaimu wa Balozi wa Japan hapa nchini,Bw. Hiroyuki KUBOTA alisema shule hii iliweza kuanzishwa kwa  msaada kutoka kwa Bw. Nakayama wa Japan ambaye alichangia hela za ujenzi wa shule.  Aliongeza kuwa Ubalozi wa Japan hapa nchini umekuwa ukisaidia shule katika masuala mbalimbali ikiwemo maboresho ya sick- bay, maabara, na kwa sasa ubalozi unasaidia upanuzi wa jengo la utawala ambao utamalizika baada ya muda mfupi.
Shule ya Sekondari ya WAMA- Nakayama iliyopo  Nyamisati, Rufiji katika Mkoa wa Pwani ilianza rasmi mwaka 2010. Shule inasaidia wasichana yatima na waliotoka katika mazingira hatarishi kutoka mikoa yote Tanzania bara na visiwani. Jumla ya wanafunzi wa kike 27 watamaliza kidato cha sita mwezi mei mwaka huu katika michepuo ya ECA  na PCB.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni