Jumatatu, 1 Agosti 2016

UGONJWA WA KIPINDUPINDU BADO UPO JIJINI DAR ES SALAAM

KIPHussein Makame-MAELEZO
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amesema ugonjwa wa kipindupindu bado upo jijini Dar es Salaam baada ya wagonjwa wapya wanne kugundulika katika Manispaa ya Temeke jijini hapa.
Waziri Ummy ameyasema hayo leo ofisini kwake jijini Dar es Salaam, wakati akitoa taarifa kwa waandishi wa habari juu ya magonjwa ya milipuko na magonjwa mengine nchini.
Alisema mwenendo wa ugonjwa huo kuanzia Julai 2016 ulikuwa wa kuridhisha kwani wagonjwa walipungua hadi kufikia 173 kwa mwezi bila kifo kutoka wagonjwa 555 walioripotiwa mwezi Juni 2016 na vifo vya watu saba.
“Mkoa wa Morogoro ni mkoa pekee umekuwa ukiripoti wagonjwa wa kipindupindu kwa kipindi kirefu hadi sasa.Vilivile mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa haujaripoti wagonjwa tangu Mei 19, 2016 ila wiki iliyopita siku ya Jumamosi waliripotiwa  wagonjwa wapya wanne katika wilaya ya Temeke” alisema Waziri Ummy.
Alisema katika kipindi cha wiki iliyopita idadi ya wagonjwa wa kipindupindu imeongezeka hadi wagonjwa 41 kutoka wagonjwa 30 wa wiki iliyotangulia ingawa hakuna aliyepoteza maisha.
“Hivyo kuna dalili za kuwepo tena ongezeko la ugonjwa wa kipindupindu jambo ambalo linafanyiwa kazi kwa haraka sana na Wizara yangu” alisema.
Alifafanua kuwa Wizara yake imeelekeza nguvu kubwa kuendelea kuudhibiti ugonjwa huo hapa Dar es Salaam na huko mkoani Morogoro na inafuatilia ugonjwa wa kuharisha katika mikoa mingine ili kubaini kama kuna mgonjwa yeyote wa kipindupindu na kuudhibiti mapema.
Aliongeza kuwa kikosi kazi cha Taifa kinaainisha maeneo makuu ya kuyafanyia kazi mkoani Morogoro ambapo yatajumuisha elimu kwa jamii, uvumbuzi wa namna gani ya kupatikana maji safi na salama na matumizi vya vyoo bora.
Mbali na kueleza mikakati hiyo, Waziri Ummy alisisitiza mikoa na halmashauri zote nchini kuendelea kutoa taarifa sahihi na kwa wakati kuhusu ugonjwa huo ili kuweza kuudhibiti endapo utabainika kuwepo sehemu yoyote nchini.
Alisema timu ya wataalamu kutoka ngazi ya Taifa ilifanya tathmini mnamo Juni, 2016 na kubaini upungufu katika utoaji taarifa katika baadhi ya mikoa na hivyo Wizara yake inashirikiana na TAMISEMI kuhakikisha inafanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa.
Ugonjwa wa kipindupindu ulianza nchini tarehe 15 Agost mwaka 2015 na hadi kufikia tarehe 31 Julai, 2016 watu 22,375 wameugua na kati yao wagonjwa 345 walipoteza maisha.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni