Serikali ya Mapnduzi ya Zanzibar imeanza kutekeleza agizo la Rais wa Zanzibar kuwalipa wazee posho

Na Masanja Mabula –Pemba
SERIKALI ya Mapnduzi ya
Zanzibar imeanza kutekeleza agizo la Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi Dk Ali Mohammed Shein la kuwalipa posho la shilingi
20,000/- wazee wote wenye umri kuanzia miaka 70 .
Katika Wilaya ya Wete zoezi
hilo limefanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jamhuri ambapo zaidi ya
wazee 200 , kutoka shehia ya Sellemu , Kipangani , Limbani , Mtemani ,
Bopwe na Utaani walijitokeza kwa ajili ya kulipwa posho hizo .
Wakizungumza na mwananchi jana
nje ya Ukumbi huo kwa nyakati tofauti , baadhi ya wazee wamemshukuru
Rais wa Zanzibar kwa kutimiza kwa vitendo ahadi yake aliyoitoa wakati
wa kampeni zilizofanyika mwaka jana .
Wamesema kuwa Serikali
imetimiza wajibu wake kwa wananchi , na kuongeza kwamba posho hilo
litawasaidia katika kutatua changamoto zinazowakabili katika familia zao
.
Khamis Rajabu Msellem (73)
alisema kwamba pamoja na changamoto zilizopo lakini Rais Shein
anapaswa kuangalia zaidi mwelekeo wa Serikali yake pamoja na maendeleo
ya wananchi anaowaongoza .
“Kwa hili Serikali imetimiza
wajibu wake wa kutukumbuka sisi wazee , kiwango cha shilingi 20,000/=
kinatosha sana kumtatulia mzee baadhi ya changamoto , kwa mpango huu
sina budi kumpongeza Rais wetu ”alisema Mzee Khamis mkaazi wa Bopwe.
Naye Time Khalfan Khamis (72)
amesifu mpango kwani hauna chembe ya ubaguzi na kuwataka wananchi kuunga
mkono juhudi za rais shein kwani zimelenga katika kuwakomboa wazee
kwani baadhi yao wamekosa msaada kutoka kwa familia zao.
Alisema miaka ya nyuma kila
mzee alikuwa akipewa posho la shilingi mia tano (500) kwa mwezi kiwango
ambacho kilikuwa hakimsaidii Mzee katika kutatua changamoto za maisha .
“Awali tulikuwa tunapewa
shilingi 500/= kwa mwezi hela ambayo ilikuwa inatumika kununulia tumbaku
na kumalizika , lakini hii leo tunapewa 20,000/= alhamdulilah
tunamshukuru Rais wetu ”alieleza Time mkaazi wa Mtemani .
Aidha Mzee Mcha Omar Bweni
(74) alisema wazee waliowanyonge wamepata nafuu wa maisha , na kuongeza
kwamba licha ya fedha hizo kuwa haiwezi kabisa kumaliza shida na
matatizo yanayowakabili .
Naibu wa Sheha wa Shehia ya
Sellem Shaban Mpangile aliliambia mwananchi kwamba zoezi hilo linaenda
kwa amani na utulivu na kila mzee aliyeandikishwa baada ya kutimiza
masharti atanufaika na mpango huo .
Alisema zoezi la ulipaji wa
posho kwa wazee wenye umri kuanzia miaka 70 , linakwenda kwa mpangilio
na utaratibu maalumu ambapo baadhi ya shehia watalipwa kesho (leo) na
hii imepangwa ili kupunguza masongamano.
“Zoezi hili limegawanywa kwa
zone , ambapo baadhi ya shehia zitakuja kesho (leo) na hii imepangwa
makusudi ili kupunguza masongamano ”alifahamisha Mpangile .
Utaratibu huu utawafanya wazee
kupokea kiasi cha shilingi milioni moja na laki mbili kwa mbili
(1,200,000/=) kwa kipindi cha miaka mitano ya uongozi wa Dr Ali Mohammed
Shein .
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni